Friday, January 29, 2010

Mwanza waipania Simba

Na Jacqueline Massano

KAMANDA wa Polisi wa mkoa wa Mwanza, Jamal Rwambow amesema iwe isiwe ni lazima timu ya Toto African iifunge Simba ili kujinusuru isishuke daraja kutokana na kuwa na pointi chache kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara inayoendelea kwenye vituo mbalimbali.
Simba inayoongoza kwenye msimamo wa Ligi kwa kuwa na pointi 39 inatarajia kushuka dimbani kesho kumenyana na Toto kwenye mechi inayotarajia kufanyika kwenye uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza.
Kamanda Rwambow alisema kutokana na jitihada walizozifanya za wananchi kuichangishia timu hiyo ili isishuke daraja ana imani inaweza kuifunga Simba siku hiyo ya Jumapili.
"Simba haiwezi kutoka Mwanza, iwe isiwe ni lazima ifungwe tu. Haiwezekani ije Mwanza halafu iondoke na ushindi huku kwetu," alisema Kamanda huyo ambaye pia ni shabiki mkubwa wa Simba.
Rwambow alisema kama timu hiyo iliweza kuifunga Simba msimu uliopita ilipoenda kucheza Mwanza, na sasa hivi wanataka kuendelea kuifunga tena. "Mzunguko wa kwanza ilitufunga kwa sababu ilikuwa Dar lakini nawaambia hivi tutawafunga tena. Ni kweli mimi naipenda Simba lakini ni lazima tuifunge," alisema
Alisema juhudi zote hizo ni kuinusuru timu hiyo ili iweze kucheza ligi kuu na kuwafanya wakazi wa Mwanza waweze kuziona timu za Simba na Yanga zikienda Mwanza kucheza soka na wala si vinginevyo.
"Tukifanya mchezo wakazi wa Mwanza watakuwa hawazioni tena timu za Simba na Yanga, na ndiyo maana na wenyewe waliamua kuichangia na kuisaidia Toto pale ilipokwama na hii yote ni kuitaka timu yao ibaki kwenye ligi," alisema
Alisema kwa sasa timu yao ina pointi nane kwenye msimamo wa ligi, kutokana na hali hiyo watafanya juhudi ili iliweze kushinda mechi zake zote saba ambazo anachezea nyumbani. "Tuna mechi saba nyumbani, hizi ni lazima tushinde, na tukishinda zote tutakuwa na pointi 28 hivyo itakuwa si rahisi kushuka daraja tena," alisema
Kamanda huyo alisema ikiwa itashindikana na timu ikashuka daraja watakuwa hawana jinsi itabidi waombe radhi kwa wakazi wa Mwanza na kujipanga upya ili timu iweze kupanda daraja tena.

Sunday, January 3, 2010

Stars vs Ivory Coast leo

#Wadau waitabiria makubwa Stars

WADAU mbalimbali wa soka nchini, wameitabiria timu yao ya taifa, Taifa Stars itajifunza mambo mengi ya kisoka pale itakapocheza mechi ya kimataifa ya kirafiki dhidi ya 'Tembo' wa Ivory Coast. Mechi hiyo inayosubiriwa kwa hamu kubwa na wapenzi wa soka nchini, itafanyika katika uwanja wa Taifa saa 1.30 usiku.
Mshauri wa timu ya soka ya Villa Squad ya Dar, Kenneth Mwaisabula, alisema mechi hiyo ni fursa nzuri kwa wachezaji wa Stars kujifunza mambo mengi kutoka kwa wapinzani wao.
"Ivory Coast ina wachezaji wengi wa kulipwa, wanafahamu mbinu mbalimbali za soka, hivyo vijana wetu wanatakiwa kuwa makini na kuangalia makosa yao ili waweze kujifunza toka kwa wenzao," alisema Mwaisabula.
Alisema mechi dhidi ya timu kubwa zenye wachezaji wa kulipwa, ni nzuri kwa timu zetu kwa kuchukua mbinu na mafunzo toka kwao na kuepukana na soka la kizamani.
mdau mwingine wa soka, Nassor Duduma katibu msaidizi wa zamani wa Yanga, alisema mechi ya leo ina malengo tofauti kwa wachezaji wa timu zote mbili huku Ivory Coast ikiwa katika maandalizi ya fainali za mataifa ya Afrika huko Angola na Stars kujifunza.
"Stars lengo lake katika mechi hiyo ni kuonyesha wanaweza na kujifunza kwa kupambana na Drogba (Didier) na Toure (Kolo), lakini wageni wanaangalia zaidi katika fainali za kule Angola," alisema Duduma.
Wakati Duduma akisema hayo, mdau mwingine wa Jijini Mwanza, Jamal Rwambow, alisema mchezo wa leo ni muhimu kwa Stars kwa sababu utatoa nafasi ya wachezaji wetu kujifunza mengi.
"Siwapi nafasi Ivory Coast ya kutushinda, lakini naamini tunaweza kutoka sare ama kushinda mechi hiyo," alisema Rwambow ambaye ni Kamanda wa Polisi mkoani Mwanza.
Aidha, alisema wachezaji wa Stars wanatakiwa kujiamini na kucheza bila woga na kuweza kuepuka majina ya wachezaji wakubwa wanaocheza soka Ulaya.
Hata hivyo, kocha maarufu nchini, Syllersaid Mziray, alipotakiwa kuzungumzia mechi hiyo, alisema kwa ufupi "Sina la kuzungumza".
Mziray ambaye amekuwa akiipinga mechi hiyo kwa madai Stars haitajifunza lolote, safari hii ameonekana kuwa mkimya zaidi.

Tuesday, December 29, 2009

Simba kuteta mwishoni mwa wiki

#Ni kujadili mabao mawili ya Yanga
Na Badru Kimwaga
VIONGOZI wa klabu ya Simba wanatarajia kuwekana 'kitimoto' na kujadili kipigo cha Yanga katika kikao chao cha Kamati ya Utendaji kitakachofanyika mwishoni mwa wiki.
Viongozi na wajumbe wote wa Kamati ya Utendaji wameshajulishwa kikao hicho muhimu, ambacho pia kitatoa nafasi ya kujadili mambo mengine muhimu ya maendeleo ya klabu.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka ndani ya klabu ya Simba, ni kwamba kikao hicho ambacho ni muendelezo ya kikao kilichofanyika awali Novemba 30 kitafanyika kwenye hoteli ya Regency.
Kubwa litakaloongelewa kwenye kikao hicho ni kipigo toka Yanga, uchaguzi mkuu na hoja ya mapato na matumizi ambayo imekuwa ikilalamikiwa kwa muda mrefu sasa.
Kamati hiyo inaundwa na Ayoub Semvua, Omar Gumbo, Mohammed Mjenga na Hassan Othman 'Hassanoo', iliyopewa kazi ya kukutana na TFF kwa lengo la kufanyia marekebisho ya katiba yao kabla ya kuitishwa kwa uchaguzi mkuu.
Mmoja wa wajumbe wa kamati ya utendaji, Said 'Seydou' Rubeya, alithibitisha kupata barua ya mualiko wa kikao hicho na kusisitiza anaenda kwenye kikao hicho kutaka majibu ya ombi lake juu ya mapato na matumizi ya klabu yao.

Kipigo kingine chaisubiri Simba

*Yanga yatamba
Na Jacqueline Massano

KATIKA mwendelezo wa kunogewa na furaha ya ushindi dhidi ya watani wao wa jadi Simba, mabingwa wa soka nchini, Yanga imesema ingetamani kupata nafasi nyingine ya 'kuionea' Simba wakati wa michuano ya Kombe la Mapinduzi inayotarajia kuanza baadaye mwezi ujao Visiwani, Zanzibar.
Yanga ilimaliza uchovu wa kutoondoka na furaha kila inapokutana na Simba baada ya kuwanyuka Wekundu hao wa Msimbazi mabao 2-1 katika mechi ya dakika 120--nusu fainali ya michuano ya Kombe la Tusker iliyomalizika kwa Yanga kutwaa ubingwa.
Simba, mabingwa wa soka nchini, Yanga na Mtibwa zitashiriki kutoka Bara, wakati wenyeji timu za Kisiwani Zenji ni pamoja na Malindi, Miembeni, Jamhuri, Zanzibar Ocean View na Mafunzo.
Afisa Uhusiano wa Yanga, Louis Sendeu amesema kuwa kikosi chako kwa sasa kiko imara kukabiliana na timu yoyote, na italeta furaha kama watakutana tena na Simba kwenye michuano hiyo.
Katika michuano ya Tusker, Simba ilimaliza kwa kushika nafasi ya tatu, kufuatia ushindi wa jasho jingi lililokauka baada ya dakika 120 na kupata ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Tusker ya Kenya katika mechi ya nusu fainali, huku Tusker ikikosa nafasi hiyo kiduchu baada ya kuwa mbele bao 1-0 mpaka dakika za majeruhi kabla ya Simba kusawazisha na kupelekea nyongeza ya dakika.
Alisema kuwa ushindi mafanikio mazuri waliyopatra kwenye michuano ya Tusker imefungua njia zaidi ya ushindani hasa katika michuano ya Ligi Kuu.
"Kama tutapangwa kundi moja na Simba, au ikatokea kukutana katika hatua yoyote, basi hii ndiyo furaha yetu. Kwa sasa tunaweza kuifunga Simba tunavyotaka. Ilikuwa makosa kudhani kwamba Simba haifungiki," alisema.
Wakati Yanga wakikosa mapumziko baada ya michuano ya Tusker, wapinzani wao Simba wako mapumzikoni mpaka Januari 2. Kwa mujibu wa Sendeu, timu yao inaanza mazoezi leo kwenye uwanja wa Shule ya Kimataifa ya Tanganyika, IST.
Hata hivyo taarifa za hofu kwamba Simba huenda isishiriki michuano hiyo, zimezimwa leo baada ya kuthibitisha ushiriki wao kupitia mtoa habari Clifford Ndimbo.
Ndimbo amesema kuwa, klabu yao itashiriki michuano hiyo kama ilivyopangwa, na kwamba wanatarajia kuanza mazoezi muda mfupi baada ya kurejea kocha Patrick Phiri aliyerudi zambia kwa mapumziko mafupi.

Monday, December 28, 2009

SOFAPAKA yawanyatia wawili wa Mtibwa


KLABU ya soka ya SOFAPAKA kutoka Kenya, imewazimia wachezaji wawili wa timu ya Mtibwa Sugar.
Fununu zilizoifikia blog hii ni kwamba uongozi wa klabu hiyo umeridhishwa na kiwango kilichoonyeshwa na mabeki hao wa Mtibwa.
Wachezaji hao ambao wanaweza kulamba bingo hilo iwapo yatafikiwa makubaliano kati ya uongozi wa Mtibwa na Sofapaka ni Idrisa Rajabu na Abdulhim Amour.
Habari zilizopatikana ni kwamba endapo uongozi huo utafanikiwa kuwasajili wachezaji hao itawatumia kwa ajili ya mashindano ya Klabu Bingwa Afrika.

Yanga yaitisha Simba

UONGOZI wa klabu ya Simba umekiri mahasimu wao Yanga walistahili kutwaa ubingwa wa michuano ya kombe la Tusker kutokana na kujiandaa vizuri kuliko wao.
Aidha, uongozi huo umewataka wanachama wao kuacha kumsaka mchawi kwa matokeo yaliyowatokea katika michuano hiyo iliyomalizika jana, na badala yake kutakiwa kushikamana kwa ajili ya mzunguko wa pili wa Ligi Kuu nchini.
Katibu Msaidizi wa klabu hiyo, Mohammed Mjenga, alisema watani wao walionekana kubadilika kisoka kwa kucheza mpira wa pasi na kwa kiwango hicho walistahili kuwa mabingwa wa Tusker.
Mjenga alisema ni dhahiri Yanga walijiandaa vyema kwa michuano hiyo tofauti na Simba na ndio maana waliweza kuibuka washindi katika mechi yao na hawana la kusingizia zaidi ya kuridhika na matokeo.
Alisema hata hivyo pamoja na kuwapa heko watani zao, bado binafsi anawatupia lawama waamuzi kwa kuonyesha udhaifu katika michuano hiyo."Tatizo la waamuzi ni sugu na hatujui litaisha lini, ni kama hawajui wajibu wao wawapo uwanjani," alisema Mjenga.
Pia aliwataka wanachama wa Simba kuacha kumsaka mchawi kutokana na matokeo ya mechi yao na Yanga na badala yake kushikamana pamoja kwa ajili ya kujiandaa na duru la pili la ligi kuu pamoja na Kombe la Shirikisho.
Mjenga alisema, lawama kwa sasa wakati muafaka, ila umoja na mshikamano pamoja na kumsapoti kocha na wachezaji kwa michuano iliyopo mbele yao ndio kitu cha muhimu zaidi.

Simba wamgeuzia kibao Phiri

BAADA ya kuchapwa mabao 2-1na mahasimu wao Yanga katika mechi ya nusu fainali ya kombe la Tusker, Simba sasa wameamua kumgeuzia kibao kocha wao mkuu, Mzambia Patrick Phiri.
Baadhi ya mashabiki, wapenzi na manazi wa timu hiyo wamesema kocha huyo ndiyo sababu kubwa ya kufungwa na Yanga, na kisha wachezaji kucheza chini ya kiwango katika michuano hiyo iliyomalizika kwa klabu hiyo ya mtaa wa Jangwani kutwaa taji.
Wakizungumza baada ya pambano lao la Alhamisi kumalizika, wapenzi hao wa Simba wakasema kitendo cha Phiri kuondoka na kwenda mapumzikoni nyumbani kwao Zambia na kuwapa mapumziko ya muda mrefu wachezaji, ndiyo sababu iliyosababisha wachezaji hao kuporomoka viwango.
"Kama kocha angekuwepo kambini na timu huko Zanzibar na kutoa mazoezi kama yale anayowapa katika Ligi Kuu Bara, basi wana imani wasingefungwa na kunyanyaswa na Yanga uwanjani na pia kuchukua ubingwa," alisema Muhidin Parojo mnazi wa Simba.
Simba timu inayochukuliwa kama ni kioo cha michuano hiyo, imecheza katika kiwango duni na kuwashangaza mashabiki waliozoea kuiona ikicheza Ligi Kuu mechi 11 bila kufungwa wala kutoka sare."
Katika mechi ua kusaka mshindi wa tatu, Simba waliishinda Tusker kwa mabao 2-1 na kushika nafasi ya tatu.Mashabiki wengi wamemtaka kocha Phiri kutowapa mapumziko tena wachezaji wake na badala yake awafanyishe mazoezi makali mara baada ya mwaka mpya kuanza.